Ijumaa, 22 Januari 2016

Weusi tusipojikubali tutaendelea kuitwa tumbiri wanaozungumza.



“Angalia katika nchi za kiafrika kama Kenya, wale watu huziibia nchi zao na kwenda kuwekeza katika nchi za nje...Hawa ni watu wanaoagiza kila kitu kutoka nje mpaka na njiti za kiberiti. Kwa mawazo yangu, nchi nyingi za kiafrika zilitakiwa ziendelee kutawaliwa kwa miaka 100 kwa sababu hawajui lolote kuhusu utawala bora”. ni maneno kutoka kwa Donald Trump, bilionea linaloomba ridhaa kugombea urais wa Marekani mwakani kupitia cha chama cha Republican. Jamaa linadharau “kinoma!”.  Kwamba sisi tunaagiza kila kitu kutoka nje hadi njiti za kiberiti. Hivi ni kweli njiti za Kiberiti sizinatengenezwa Mufindi? Kwamba tulitakiwa tuendelee kutawaliwa na wakoloni.  Linatukumbusha “ukuda” wa Waingereza walipotuchongea huko umoja wa Mataifa kwamba Tanganyika haijawa tayari kujitawala labda mpaka mwaka 2059. Tumshukuru Mungu Mzee Nyerere “alikomaa” mpaka kikaeleweka. Leo tunasherehekea miaka 52 ya Uhuru pamoja na kwamba bado tumevaa nepi. Lakini hivi ni kwa nini? Yaani karibu nchi zote za Afrika zimevaa nepi na uzee wote huo. Aibu! Shida ni matendo yetu. Matendo yameyopelekea tutukanwe na tukatukanika. Nitasema tu!


Kati ya weupe wote waliowahi kumtukana mtu mweusi, aliyevunja rekodi ni aliyekuwa  mfalme wa ubaguzi wa rangi enzi hizo Afrika Kusini, Peter Botha. Mwaka 1985 akilihutubia baraza lake la mawaziri alitutukana eti weusi hatuna lolote jema, isipokuwa mashujaa wa kupiga kelele, kucheza ngoma, kuoa wanawake wengi na kupenda sana ngono. Kwamba mtu mweusi ni alama ya umaskini, udumavu wa akili, uvivu na aliyekosa ushindani”. Botha alikuwa mjinga kweli. Yaani na ufalme wake wote alishindwa kuelewa kwamba kusema ukweli Afrika ni dhambi! Au hata wewe unayenisoma hujui kama kusema ukweli katika nchi ambazo viongozi huwaibia watu wao kusema ukweli ni kosa? Kama huamini muulize Mnyika kilichompa pale aliposema kiranja wa nchi yake ni dhaifu.


Lakini pengine tabia za kucheza, kupenda ngono na utawala wa ubabaishaji utakuwa unatuhusu. Nasema Hata Comte Joseph – Arthur Gobineau miaka ya 1800 amewahi kuandika kwamba waafrika ni watu wanaokosa ubunifu wa kisanyansi na kisiasa badala yake wanafaa zaidi kwa kazi ya kucheza, kuvaa na kuimba alipata msuko. James Watson, mwanasayansi maarufu sana duniani na mshindi wa nishani ya Nobel katika tiba mwaka 1962, aliwahi kusema pia mtu mweusi ana akili kidogo kuliko mtu mweupe. Lakini swali la msingi ni kwa nini matusi hayo yaelekezwe kwa weusi tu? Unajua ukisoma vizuri kitabu cha Chancellor Williams, “Destruction of Black Civilization: Great Issues of a Race from 4500 B.C. to 2000 A.D” utagundua weusi ndo tulikuwa mbele kwa kila kitu. Tulifanya mambo makubwa sana yaliyothibitisha kwamba uwezo wetu wa kufikiri ulikuwa juu. Je tulipotea wapi? Kwa sababu haiwezekani watu mashuhuri wautilie shaka uwezo wetu wa kufikiri.


Siku za nyuma mawaziri kadhaa waJapan walipata kusema kwamba wanatilia shaka uwezo wa mtu mweusi katika kufikiri. Yaani huyu pamoja na kwamba weusi tunashindana kununua magari ya Japani na bidhaa nyingine bado anatilia shaka uwezo wetu wa kufikiri? Au ni hayo magari ya bei mbaya tunayoshindana kuwanunulia viongozi wetu na wakati viongozi wetu hawaishi kupigana vikumbo huko ughaibuni kuomba omba? Chika Onyeani katika kitabu chake cha Capitalist Nigger naye anashangaa ni kwa nini Mwafrika atukanwe namna hiyo na mawaziri wa Japan lakini bado waendelee kununua bidhaa toka Japan. Chika alitegemea tungesusia mabidhaa ya kutoka Japan.


Sidhani kama kususia bidhaa inatosha na badala yake tuyatathimini matendo yetu. Tubadilishe tunavyoenenda. Tuache kwenda kama Tumbiri.   Manyanyaso,matusi na kila aina ya dharau vitaisha pale tu tutakapo jitambua, kujiheshimu na kujikubali.  Kwa nini nasema hivyo? Tumevunja rekodi katika kutafuta ufahari wa kijinga na kusahau mambo ya maana. Profesa Ali Mazrui amewahi kuandika, “Mwafrika hawezi kuwa mshiriki mzuri katika ubinafsishaji kwa sababu hana utashi na ari ya kupata faida na ulimbikizaji badala yake anatawaliwa na majivuno na ufahari; ni mfanyabiashara mbaya  asiyeweza kutegemewa”.Yaani tunaona fahari kwenda kuombaomba na kujidhalilisha mbele ya wazungu na wakati tunakila kitu. Hata wao wanachoshwa na tabia zetu za ombaomba. Jenerali Ulimwengu amewahi kuandika kwamba  kinachowaudhi wazungu zaidi ni tabia yetu ya kuombaomba inayoambatana na ubadhirifu wa kutisha. Hawaelewi ni jinsi gani nchi inaweza kutembea kote duniani ikiombaomba kwa kusafiri daraja la kwanza wakati wafadhili wenyewe wanasafiri daraja la kawaida. Ni kama ombaomba uliyemtupia shilingi mia tano hapo mapema umkute hotelini anafurahia ‘lobster’ na mvinyo. Ulimwengu huwa anamaneno!

Ukweli ni kwamba tunafanya upuuzi kwa sababu wazungu wametutikisa kidogo tukanywea, tukajiona sisi kweli ni washenzi na ishara ya laana na umaskini. Tukajikuta tunamtukuza mzungu. Leo hii mtu mzima anaona ustarabu ni kuwa na rafiki mzungu, kuishi ulaya na kufanana na mzungu. Hiyo ndiyo definition ya maisha tuliyonayo. Carter G. Woodson katika kitabu chake kiitwacho, “Miseducation of the Negro” anasema, “If you can control a man’s thinking you do not have to worry about his action. When you determine what a man shall think you do not have to concern yourself about what he will do. If you make a man feel that he is inferior, you do not have to compel him to accept an inferior status, for he will seek it himself”. Wazungu wametufanya washenzi nasi tukakubali na kwa nguvu zote tukawekeza katika kujikana wenyewe na kuwa wazungu. Hakuna anayekulazimisha kujichubua, hakuna anayekulazimisha kuvaa manyoya kichwani, hakuna anyekulazimisha kuongea kama wazungu. Utajikuta unafanya mwenyewe, tena kwa gharama za juu. Woodson anakwambia, “If you make a man think that he is justly an outcast, you do not have to order him to the back door. He will go without being told; and if there is no back door, his very nature will demand one and cut one to enter”.Hiyo ndiyo siri pekee anayoitumia mtu mweupe kumshenzisha mtu mweusi.


Leo hii hata ukijaribu kuongea Lugha yako ya asili lazima utachekwa tu na pale utakapoogea Lugha ya Mzungu utasifiwa na kila mtu. Lugha zetu za asili tunaziita vernacular languages. Jamaa yangu mmoja amekata channels zote za kizungu kwenye luninga yake na kununua katuni zinazozungumza kizungu tu kwa lengo la kwamba watoto wake waongee kizungu. Matokeo yake watoto wanakula kama katuni, wanacheza kama katuna na kuongea kama katuni. Pale nyumbani hawasikilizani. Sasa kwa mwendo huu tukiitwa tumbiri wanaozungumza tutamlaumu nani?

Matusi haya siyo ya bure, ni kwa sababu ya mienendo yetu. Sisi pamoja na usomi wetu bado tu hamnazo. Yaani kila elimu inavyozidi kuongezeka ndivyo mtu mweusi anavyozidi kujikataa. Angalia wasomi wote, wanashangaza. Pengine ndiyo maana inasemekana “ Ni rahisi sana kumtawala msomi wa Kiafrika kuliko Mwafrika asiye na kisomo, kwa sababu Mwafrika asiye na kisomo anamwamini sana  ndugu yake aliyesoma”. Kujikataa kote huku kumeletwa na wasomi. Jenerali Ulimwengu anasema, “Tunauchukia Uafrika, na ingekuwa inawezekana tukaumbwa upya katika muonekano mwingine, bila shaka tungeteua kuwa Wazungu au Waasia, au Waeskimo, kwa jinsi tunavyoona dada zetu – wakati mwingine hata wanaume – wakijichubua ili wawe na ngozi nyeupe. Leo hii, zaidi ya nusu ya wanawake unaokutana nao wamefunga manyoya kichwani yanayofanana na nywele za Kizungu au Kiasia. Manyoya haya, ambayo ni ya gharama kubwa, yananunuliwa hata na wanawake ambao hawajui mlo ujao utatoka wapi, lakini fasheni ni kuwa Mzungu bandia, na hilo ni muhimu kuliko chakula”.


Yaani ukiisha ikamata akili ya mwanadamu huna haja ya kutumia nguvu nyingi kumuelekeza kujikataa. Ulimwengu anaendelea kuzungumza kupitia maandisha yake, “Tumeambiwa mara kwa mara kwamba kuchubua ngozi ni hatari kwa afya yako kwani kunasababisha ngozi iathirike na mionzi ya jua, na hilo linaweza kusababisha saratani, lakini hatusikii, kwa kuwa labda ni bora uwe Mzungu kwa muda mfupi halafu ufe kuliko kuishi miaka mingi bila kuwa Mzungu walau kidogo. Manyoya yanayovaliwa na akina mama wakati mwingine huja yakiwa yamebeba chawa na minyoo, na ni rahisi kwa wadudu hawa kuwaumiza wavaaji wa manyoya hayo”. Ndiyo maana Malcom X anakuuliza, “Who taught you to hate the texture of your hair? Who taught you to hate the color of your skin? To such extent you bleach, to get like the white man. Who taught you to hate the shape of your nose and the shape of your lips? Who taught you to hate yourself from the top of your head to the soles of your feet? Who taught you to hate your own kind? Who taught you to hate the race that you belong to so much so that you don't want to be around each other?”.

Wazungu wanatuangalia na wanatufuatilia katika kila tunalofanya, na kwa kuwa wanajua kwamba tunajidharau, nao hawana la kufanya ila kutudharau. Walitwambia kwamba ili tuinue uchumi wetu tunatakiwa kuondoa ruzuku na tukakubali. Wakati  ng’ombe mmoja wa Ulaya analipwa  ruzuku ya dola za Marekani kwa siku, huku kwetu wafugaji ndiyo wamekuwa mitaji ya maafisa mifugo. Kila akimchoma ng’ombe wako sindano ya chanjo lazima umlipe.  Sasa ukihesabu gharama za ufugaji lazima uachane na shughuli hiyo.  Erik Reinert kupitia kitabu chake, “How Rich Countries Got Rich . . . and Why Poor Countries Stay Poor” anatoa ushauri kwa nchi maskini kwamba zisifanye kile ambcho nchi tajiri wanasema, bali wafanye kile nchi tajiri wanachofanya. Pamoja na ushauri wote huo bado tunaendelea kuiishi kwa za kuambiwa.

Kujitoa kwetu ufahamu kumeendelea kutufanya tuamini uzungu ndiyo mwarobaini wa mafanikio. Ilifikia kipindi kiranja mkuu wetu na washabaki wa mpira wa miguu kuamini kocha wa kizungu ndiyo atamaliza matatizo ya mpira ili tukawafunge Brazili. Utasikia, “Leta kocha wa kizungu, waweke vijana kambini, wapate msosi freshi, vijana watanoleka bila taabu, kisha tunakwenda kucheza Kombe la Dunia”. Hivi kwa mtindo huu tukiitwa tumbiri wanaoongea  tutachukia? Kwa mawazo mafupi namna hii kama mkia wa mbuzi mataifa makubwa, yataendelea kutuita washenzi, ma-mbumbumbu, hohehahe wasio na nyuma wala mbele.

Historia inaonyesha kwamba chuo kikuu cha kwanza duniani kilikuwa Afrika, kule Mali. Maajabu mengi yaliyofanyika Misri, yalifanywa na Weusi. Uvumbuzi wa hisabati ulitoka Afrika, hata mtu wa kwanza duniani anaaminika kuishi Afrika. Hata Yesu alikuwa mweusi! Mapapa watatu wa mwanzo kabisa walikuwa weusi. Hata Yesu Kristu, alikuwa Mweusi wa Misri, na ndiyo maana Simon wa Krene, ambaye kwenye Injili, tunaambiwa alikuwa Mweusi alimsaidia Yesu, kubeba msalaba. Ilikuwa ni huruma ya kuona Mweusi mwenzake anateswa ameandika Padri Karugendo, mwandishi nguli katika Makala kwenye gazeti la Rai Mwema. Lakini Aylmer Von Fleischer (How Jesus Christ Became White) anaandika, “One of the major reasons why the image of Jesus Christ was changed from Black to White was because of the rise of White supremacy in Europe and across the world, and the demise of the Black race. Whites were heavily involved in the destruction of many Black civilizations like the Indus, ancient Egyptian and Hebrew" Na baada ya hapo weusi wakaufananisha shetani. Hata ukiangalia katika vitabu vyao vyote shetani ni mweusi.  Hiyo ni danganya toto.  Lakini chukua muda, soma  kitabu cha, “ The Destruction of Black Civilization” kinapatikana kwenye mtandao tena kwa bure.

Akiongea na weusi wenzake Bill Cosby aliwahi kusema, “Men, if you want to win, we can win,” . “We are not a pitiful race of people. We are a bright race, who can move with the best. But we are in a new time, where people are behaving in abnormal ways and calling it normal”.  Kuzikataa nywele zako na kuvaa za mzungi ni kubehave in abnormal ways and calling it normal, kuikataa rangi yako na kujichubua kuwa kama ya mzungu ni kubehave abnormal ways and calling it normal, kutamani kuishi kama mbwa Ulaya ni kubehave in abnormal ways and calling it normal, kuwalazimisha watoto wako kuikataa lugha ya mababu zako ni kubehave in abnormal ways and calling it normal. Tubadilike. Tuache ukenge, maisha yanawezekana hapa hapa nyumbani.  Unachotakiwa ni kubadilisha namna ya kufikiri tu. Naamni ukisoma vizuri kitabu changu cha Ukombozi wa Fikra utajikubali na kuifurahia Dunia. Tukibadilika mazuri yatatoka kwetu kama asemavyo Patrice Lumumba katika barua yake ya mwisho kwa mkewe, Pauline “Siku moja Historia itajieleza; haitakuwa Historia inayotolewa Umoja wa Mataifa, Washington, Paris wala Brussels, bali ni Historia ya Afrika. Siku moja Afrika itaandika Historia yake yenyewe, Kusini na Kaskazini mwa Jangwa la Sahara kutatukuka.”

Tukiruhusu akili zetu kufanya kazi kwa kudadisi, kuhoji na kufikiri kwa kina siku moja magazeti ya Tanzania yataandika, “Tanzania itasitisha misaada yake kwa Marekani  kutokana na vitendo vya ubaguzi nchini humo”, “ India yashukuru msaada kutoka Tanzania ambao ulipanga kuwasaidia wahanga wa mafuriko ambayo inasemekana  hayajawahi kutokea tangu uumbwaji wa dunia”, Uingereza yaandaa mapokezi makubwa kumpokea Mhe, Rais kutoka Tanzania. Siyo utani, ni ukweli tu. Wazungu waliweza kuvuruga ustaraabu wa mtu mweusi kwa kucheza na akili tu. Akili ni injini ya mwili, pale inaponoki gari halisongi. Njia pekee ya kujifunza kufikiri ni kufikiri, kudadisi ni kudadisi na kuhoji ni kuhoji. Kazi ya kichwa siyo kufuga nywele ni kufikiri vizuri. Tukibadili namna ya kufikiri, tukajenga utamaduni wa kuhoji na kudadisi naapa Tanzania itakuwa na watawala wanaoendesha nchi yetu  katika misingi ya akili na mantiki, ikiwa na viwanda vya kutengeneza bidhaa badala ya kuuza mali-ghafi. Tutaacha kusafirisha ajira za vijana wetu kwenda China na mali-ghafi zetu zitatumika kuzalisha ajira hapa hapa  Tanzania  kwa ajili ya vijana wetu. Tutakuwa nchi ya viwanda, utafiti, uvumbuzi, usomi uliotukuka, na falsafa ya kina. Tutaondokana na njaa, maradhi na umasikini katikati ya neema kubwa. Watu wetu wataishi maisha ya staha na furaha. Watoto wetu, wanawake wazazi na wazee watakuwa na siha bora maisha yao yote.


Tukifikia hatua vijana wa kizungu watatuheshimu kwa sababu tutajulikana kama watu makini, watu wenye mantiki, siyo ombaomba. Watakuja kujifunza kutoka kwetu kwa sababu tutakuwa tunafanya maajabu. Watatamani kuwa weusi. Watabadili hata nywele zao kuwa kama zetu. Tujenge utamaduni wa kuhoji kwa kila kitu ili tusiwe kama waziri mmoja wa Tanzania waziri mhusika wa sekta ya madini alitembelea machimbo ya dhahabu, akapitishwa sehemu kadhaa, lakini alipotaka kuingia chumba cha kuhifadhia dhahabu akazuiwa kwa sababu za ‘kiusalama na bila hata kuhoji alifyata mkia. Jamani kutohoji hukufanya ufyate mkia. Mshairi Marcelino Dos Santos wa Msumbiji anasema; "We Must Plant". Kwa maana ya tuna lazima ya kupanda. Dos Santos hazungumzii kupanda mbegu za mahindi au mtama, bali kupanda fikra za makini kwa wanajamii. Fikra zitakazowasaidia kutoka katika hali iliyopo na kwenda kwenye hali nyingine iliyo bora zaidi.

Jumamosi, 26 Desemba 2015

Tunahitaji Ukombozi wa Fikra

Mara baada ya kupata uhuru wa bendera, Mwl Julius Nyerere alielekeza nguvu katika ukombozi wa fikra. Mwalimu aliamini bila ukombozi wa fikra, watanzania wataendelea kuishi utumwani. Kwa hiyo alitumia elimu kupambana na utumwa wa fikra. Alipeleka vijana wengi karibu kila kona ya dunia kuitafuta elimu. Lakini kwa bahati mbaya wengi wakaenda kupambana na mitihani badala ya utumwa wa fikra. Wakarudi na vyeti bila fikra za kimaendeleo na wakageuka kuwa tishio kwa rasilimali zetu. Kwa ujumla juhudi zake za kutukomboa kifikra zikawa zimegonga mwamba. Mpaka anaiaga dunia Nyerere katuachia uhuru wa bendera tu. Uhuru ambao mwenye nacho ndiyo binadamu na asiyenacho ni taka taka. Machinga jijini Mwanza na Dar es Salaam wanaitwa taka taka. Ndiyo uhuru huo tunaojivunia watanzania. Uhuru unao wagawa watu kwa kipato na si utu. Huu siyo uhuru, ni hatua ya kwanza katika ukombozi. Hatua ya pili ni ukombozi wa fikra na ukombozi wa kiuchumi ndiyo hatua ya mwisho.

Kitendo cha kupiga deki barabarani ili wanyonyaji wapite ni ishara ya kwamba bado tu watumwa wa fikra. Kuzunguka dunia nzima kuleta wawekezaji wasiokuwa na mitaji ni utumwa wa fikra. Kuwarudisha madarakani wezi wa rasilimali zetu huku hatuna huduma za jamii ni udumavu wa fikra. Kumshangilia jamaa anayefanya uwe hivyo ulivyo leo kwa sababu tu kakupatia tsheti, kofia na pombe kidogo ni ishara ya kwamba akili zetu haziko sawa sawa. Aliyesema umaskini wa watanzania uko kichwani kwakweri hajakosea. Maajabu tunayoyafanya yanathibitisha hivyo.  Wapare wanakwambia ni heri kuchakaza nguo kuliko kuchakaza akili. Akili ikichakaa lazima utavunja rekodi katika kufanya maajabu.  Leo hii tunawalamba miguu wezi wa rasilimali zetu. Hivi kama haya siyo maajabu ni nini? Kucheka na mtu aliyesababisha hospitali zikose dawa, watoto wako wafukuzwe shule kwa kukosa ada, mazao yako kukosa soko na biashara yako kukosa faida ni uthibitisho wa wazi kwamba tuko huru gereni. Wallahi tumerogwa. Siyo bure.Haiwezekani uendelee kumsujudia mtu aliyekula hela yako ya likizo tukasema uko salama kichwani, tutakuwa tunakuonea. Unahitaji tiba! Yaani ukombozi wa fikra ili uweze kuona mambo katika uhalisia wake.

Kwa mfano, watawala dhalimu pamoja na kutukalia kichwani bado tunawapa ridhaa ya kurudi madarakani na kuwaacha wale viongozi wazuri. Haiwezekani aliyepinga ubadhirifu wa ESCROW anyimwe ubunge na wakati aliyepiga arudi bungeni kwa kishindo halafu tuseme sisi siyo wagonjwa. Tunaumwa Stockholm.  Stockholm ni ugonjwa wa kumpenda na kumtetea adui yako. Ndiyo maana nasema Nyerere aliondoka hajaimaliza kazi ya kutukomboa kifikra. Lakini kuondoka kwa Nyerere isiwe kigezo cha sisi kushindwa kuutafuta ukombozi wa fikra. Tuendelee kupamba na utumwa huo, vinginevyo tutaendelea kuogelea kwenye umaskini endelevu.  Denis Waitley aliwahi kusema,  “Maisha siku zote yamejaa hatari tu. Lakini kunahatari moja kubwa ambayo unatakiwa kuizuia kwa gharama yoyote na hiyo ni hatari ya kutofanya lolote”.Kuendelea kujitoa ufahamu kwa kuwakumbatia mafisadi ili waendelee kutafuna keki ya taifa hili ni hatari ya kutofanya lolote katika maisha yetu. Ndiyo maana nasema tunahitaji fikra ya kuweza kuyaona . Kuendelea kucheka na nyani tutavuna mabua.

Tunahitaji kuamka na kusema kutumika sasa basi. Urafiki gani wa siku za uchaguzi na kuwa taka taka baada ya uchaguzi? Hii danganya toto ya kwamba machinga ni rafiki wa watawala wakati wa kampeni ni matusi na kumbuka   akutukanaye hakuchagulii tusi. Kama huamini ninacho kisema, angalia inapokaribia uchaguzi machinga wanakuwa rafiki wa serikali. Wanauza bidhaa zao kiholela, yaani kila palipo na upenyo wapo. Baada ya uchaguzi wanageuka kuwa takataka ambazo mwisho wa siku lazima ziondoke. Atakayekaidi lazima akutane na askari mgambo. Yaani ndugu zangu askari mgambo ndo hawajitambui kabisa. Kwa posho ya shilingi 5000 yuko tayari kumpiga mlalahoi mwenzao. Jamani hata kuelewa hili tunahitaji kuwa na elimu ya chuo kikuu? Hapa ni ukombozi wa fikra tu.  

Watanzania tuko huru lakini uhuru wa bendera hautoshi. Uhuru wa bendera haufai hata kidogo. Uhuru wa bendera ni sawa na kuvaa suruali isiyo na zipo ukweni, utakuwa mtu mwenye wasiwasi, mashaka na aibu. Uhuru wa bendera umetujengea wasiwasi, na nidhamu ya woga na mwisho wa siku watawala dhalimu kuendelea kutunyonya kutokana na wasi wasi wetu. Kama ilivyo kwa  uhai wa samaki kwenye maji ndio ilivyo uhuru wa bendera kwa uhai wa wanyonyaji.  

Ndiyo maana tunahitaji kuutafuta ukombozi wa fikra na mengine tutazidishiwa. Tuhakikishe kichwani panakuwa vizuri. Kichwani pakiwa vizuri hutakuwa na haja ya kukimbizana na samaki bwawani kama unataka kuwatokomeza. Badala yake ni kuwakaushia maji yote na hapo utawakamata kirahisi sana. David J. Schwartz kupitia kitabu chake cha, “The Magic of Thinking Big” anasema, “fikra zinazoongoza akili yako ni muhimu zaidi ya kiasi cha akili ulizo nazo”.

Fikra sahihihi zinahitaji utulivu wa akili. Fikra sahihi hazihitaji papara. Kuwa na muda wa kufikiria ndilo chimbuko la uvumbuzi na maendeleo yote duniani. Maendeleo hayawezekani bila mabadiliko ya fikra na wale ambao hawawezi kubadili namna wanavyofikiri hawawezi kubadili chochote, alisema George Bernard Shaw. Tunahitaji kufikiri kwa usahihi kwa kila tunalolifanya. Tunahitaji kuwa na karakana za kufikiri akilini. Kama hulitaki jambo fulani libadilishe, kama huwezi kulibadilisha badili unavyofikiria juu ya jambo hilo alisema Mary Eugebreit. Badala ya kufikiri umaskini tulionao ni mapenzi ya Mungu tufikiri umaskini kama matokeo ya uzembe wetu. Mungu  ametupa rasilimali nyingi ambazo kama zingelitumika kwa faida yetu, zingeliweza zikatuinua tukawa matajiri. Tufikiri kwanza ndipo tutende. Kwame Nkrumah alisema, “matendo pasipo mawazo ni upofu, mawazo pasipo vitendo ni utupu”. Tunapo waachia watu wengine  madini kila kona ya Tanzania bila kuchangia vya kutosha katika maendeleo ya nchi hii ni utupu na upofu. Mungu aliyaweka madini haya nchini kwetu ili tuweze kujitajirisha na kutokomeza umasikini.

Nimalizie kwa kuwaasa watanzania wenzangu kwamba, saa ya ukombozi wa fikra ni sasa. Tusitegemee kama kuna mtu atakuja kutukomboa isipokuwa ni sisi wenyewe alisema Bob Marley, katika wimbo wake , “Redemption”. Bila fikra huru tutaendelea kushuhudia watawala dhalimu wakishindana katika matanuzi. Akinunua BWM, mwenzake ananunua Benz,sisi walala hoi tukiendelea kushughulikiwa vizuri na umaskini. Hii ndiyo itikadi ya Bongo. Inatia uchungu kwa nchi iliyokuwa nchi. Kumbuka laana au dhambi haikupi muda. Unakosa inakuadhibu pale pale. Gharama ya utumwa wa fikra ni kubwa. Tunakula adhabu kila siku. James Allen anasema, “Leo upo pale ambapo mawazo yako yamekuleta; kesho utakuwa pale ambapo mawazo yako yatakupeleka.” Mtu anavyofikiria katika akili yake anakuwa hivyo, na anavyochagua anakuwa hivyo”. Fikra finyu ni adui wa ndani.Tupambane nazo.   


Jiongezee maarifa kwa kusoma kitabu hiki na hakika utakombolewa kifikra. Mfalme Suleiman alisema, “ mtu mpumbavu ni yule asiyeona raha katika kutafuta maarifa, lakini daima ni mtu wa kuelezea mawazo yake binafsi. Akili ya mtu mwerevu hutafuta maarifa na sikio la mtu mwenye busara hutafuta kusikia maarifa. Mtu mpumbavu hufikiri njia yake ni sahihi daima, lakini mwenye busara hutafuta ushauri”.