Mara baada ya
kupata uhuru wa bendera, Mwl Julius Nyerere alielekeza nguvu katika ukombozi wa
fikra. Mwalimu aliamini bila ukombozi wa fikra, watanzania wataendelea kuishi
utumwani. Kwa hiyo alitumia elimu kupambana na utumwa wa fikra. Alipeleka
vijana wengi karibu kila kona ya dunia kuitafuta elimu. Lakini kwa bahati mbaya
wengi wakaenda kupambana na mitihani badala ya utumwa wa fikra. Wakarudi na
vyeti bila fikra za kimaendeleo na wakageuka kuwa tishio kwa rasilimali zetu. Kwa
ujumla juhudi zake za kutukomboa kifikra zikawa zimegonga mwamba. Mpaka anaiaga
dunia Nyerere katuachia uhuru wa bendera tu. Uhuru ambao mwenye nacho ndiyo
binadamu na asiyenacho ni taka taka. Machinga jijini Mwanza na Dar es Salaam
wanaitwa taka taka. Ndiyo uhuru huo tunaojivunia watanzania. Uhuru unao wagawa
watu kwa kipato na si utu. Huu siyo uhuru, ni hatua ya kwanza katika ukombozi.
Hatua ya pili ni ukombozi wa fikra na ukombozi wa kiuchumi ndiyo hatua ya mwisho.
Kitendo cha
kupiga deki barabarani ili wanyonyaji wapite ni ishara ya kwamba bado tu
watumwa wa fikra. Kuzunguka dunia nzima kuleta wawekezaji wasiokuwa na mitaji
ni utumwa wa fikra. Kuwarudisha madarakani wezi wa rasilimali zetu huku hatuna huduma
za jamii ni udumavu wa fikra. Kumshangilia jamaa anayefanya uwe hivyo ulivyo
leo kwa sababu tu kakupatia tsheti, kofia na pombe kidogo ni ishara ya kwamba
akili zetu haziko sawa sawa. Aliyesema umaskini wa watanzania uko kichwani
kwakweri hajakosea. Maajabu tunayoyafanya yanathibitisha hivyo. Wapare wanakwambia ni heri kuchakaza nguo
kuliko kuchakaza akili. Akili ikichakaa lazima utavunja rekodi katika kufanya
maajabu. Leo hii tunawalamba miguu wezi
wa rasilimali zetu. Hivi kama haya siyo maajabu ni nini? Kucheka na mtu
aliyesababisha hospitali zikose dawa, watoto wako wafukuzwe shule kwa kukosa
ada, mazao yako kukosa soko na biashara yako kukosa faida ni uthibitisho wa
wazi kwamba tuko huru gereni. Wallahi tumerogwa. Siyo bure.Haiwezekani uendelee
kumsujudia mtu aliyekula hela yako ya likizo tukasema uko salama kichwani,
tutakuwa tunakuonea. Unahitaji tiba! Yaani ukombozi wa fikra ili uweze kuona
mambo katika uhalisia wake.
Kwa mfano,
watawala dhalimu pamoja na kutukalia kichwani bado tunawapa ridhaa ya kurudi
madarakani na kuwaacha wale viongozi wazuri. Haiwezekani aliyepinga ubadhirifu
wa ESCROW anyimwe ubunge na wakati aliyepiga arudi bungeni kwa kishindo halafu
tuseme sisi siyo wagonjwa. Tunaumwa Stockholm.
Stockholm ni ugonjwa wa kumpenda na kumtetea adui yako. Ndiyo maana
nasema Nyerere aliondoka hajaimaliza kazi ya kutukomboa kifikra. Lakini
kuondoka kwa Nyerere isiwe kigezo cha sisi kushindwa kuutafuta ukombozi wa
fikra. Tuendelee kupamba na utumwa huo, vinginevyo tutaendelea kuogelea kwenye
umaskini endelevu. Denis Waitley aliwahi
kusema, “Maisha siku zote yamejaa hatari
tu. Lakini kunahatari moja kubwa ambayo unatakiwa kuizuia kwa gharama yoyote na
hiyo ni hatari ya kutofanya lolote”.Kuendelea kujitoa ufahamu kwa kuwakumbatia
mafisadi ili waendelee kutafuna keki ya taifa hili ni hatari ya kutofanya
lolote katika maisha yetu. Ndiyo maana nasema tunahitaji fikra ya kuweza
kuyaona . Kuendelea kucheka na nyani tutavuna mabua.
Tunahitaji
kuamka na kusema kutumika sasa basi. Urafiki gani wa siku za uchaguzi na kuwa
taka taka baada ya uchaguzi? Hii danganya toto ya kwamba machinga ni rafiki wa
watawala wakati wa kampeni ni matusi na kumbuka akutukanaye hakuchagulii tusi. Kama huamini
ninacho kisema, angalia inapokaribia uchaguzi machinga wanakuwa rafiki wa serikali.
Wanauza bidhaa zao kiholela, yaani kila palipo na upenyo wapo. Baada ya
uchaguzi wanageuka kuwa takataka ambazo mwisho wa siku lazima ziondoke.
Atakayekaidi lazima akutane na askari mgambo. Yaani ndugu zangu askari mgambo
ndo hawajitambui kabisa. Kwa posho ya shilingi 5000 yuko tayari kumpiga
mlalahoi mwenzao. Jamani hata kuelewa hili tunahitaji kuwa na elimu ya chuo
kikuu? Hapa ni ukombozi wa fikra tu.
Watanzania tuko
huru lakini uhuru wa bendera hautoshi. Uhuru wa bendera haufai hata kidogo. Uhuru
wa bendera ni sawa na kuvaa suruali isiyo na zipo ukweni, utakuwa mtu mwenye wasiwasi,
mashaka na aibu. Uhuru wa bendera umetujengea wasiwasi, na nidhamu ya woga na
mwisho wa siku watawala dhalimu kuendelea kutunyonya kutokana na wasi wasi
wetu. Kama ilivyo kwa uhai wa samaki
kwenye maji ndio ilivyo uhuru wa bendera kwa uhai wa wanyonyaji.
Ndiyo maana
tunahitaji kuutafuta ukombozi wa fikra na mengine tutazidishiwa. Tuhakikishe
kichwani panakuwa vizuri. Kichwani pakiwa vizuri hutakuwa na haja ya
kukimbizana na samaki bwawani kama unataka kuwatokomeza. Badala yake ni
kuwakaushia maji yote na hapo utawakamata kirahisi sana. David J. Schwartz
kupitia kitabu chake cha, “The Magic of Thinking Big” anasema, “fikra
zinazoongoza akili yako ni muhimu zaidi ya kiasi cha akili ulizo nazo”.
Fikra
sahihihi zinahitaji utulivu wa akili. Fikra sahihi hazihitaji papara. Kuwa na muda wa kufikiria ndilo chimbuko la uvumbuzi
na maendeleo yote duniani. Maendeleo hayawezekani bila mabadiliko ya fikra na
wale ambao hawawezi kubadili namna wanavyofikiri hawawezi kubadili chochote,
alisema George Bernard Shaw. Tunahitaji kufikiri kwa usahihi kwa kila
tunalolifanya. Tunahitaji kuwa na karakana za kufikiri akilini. Kama
hulitaki jambo fulani libadilishe, kama huwezi kulibadilisha badili unavyofikiria
juu ya jambo hilo alisema Mary Eugebreit. Badala ya kufikiri umaskini tulionao ni
mapenzi ya Mungu tufikiri umaskini kama matokeo ya uzembe wetu. Mungu ametupa rasilimali nyingi ambazo kama zingelitumika
kwa faida yetu, zingeliweza zikatuinua tukawa matajiri. Tufikiri kwanza ndipo
tutende. Kwame Nkrumah
alisema, “matendo pasipo mawazo ni upofu, mawazo pasipo vitendo ni utupu”. Tunapo
waachia watu wengine madini kila kona ya
Tanzania bila kuchangia vya kutosha katika maendeleo ya nchi hii ni utupu na
upofu. Mungu aliyaweka madini haya nchini kwetu ili tuweze kujitajirisha na
kutokomeza umasikini.
Nimalizie kwa
kuwaasa watanzania wenzangu kwamba, saa ya ukombozi wa fikra ni sasa. Tusitegemee
kama kuna mtu atakuja kutukomboa isipokuwa ni sisi wenyewe alisema Bob Marley,
katika wimbo wake , “Redemption”. Bila fikra huru tutaendelea kushuhudia
watawala dhalimu wakishindana katika matanuzi. Akinunua BWM, mwenzake ananunua
Benz,sisi walala hoi tukiendelea kushughulikiwa vizuri na umaskini. Hii ndiyo
itikadi ya Bongo. Inatia uchungu kwa nchi iliyokuwa nchi. Kumbuka laana au
dhambi haikupi muda. Unakosa inakuadhibu pale pale. Gharama ya utumwa wa fikra
ni kubwa. Tunakula adhabu kila siku. James Allen anasema, “Leo upo pale ambapo mawazo yako yamekuleta;
kesho utakuwa pale ambapo mawazo yako yatakupeleka.” Mtu anavyofikiria katika akili yake anakuwa
hivyo, na anavyochagua anakuwa hivyo”. Fikra finyu ni adui wa ndani.Tupambane
nazo.
Jiongezee
maarifa kwa kusoma kitabu hiki na hakika utakombolewa kifikra. Mfalme Suleiman
alisema, “ mtu mpumbavu ni yule asiyeona raha katika kutafuta maarifa, lakini
daima ni mtu wa kuelezea mawazo yake binafsi. Akili ya mtu mwerevu hutafuta
maarifa na sikio la mtu mwenye busara hutafuta kusikia maarifa. Mtu mpumbavu hufikiri
njia yake ni sahihi daima, lakini mwenye busara hutafuta ushauri”.